
Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaaam
MKURUGENZI Msaidizi, Kitengo cha Afya Moja, Ofisi ya Waziri Mkuu, Dkt. Salum Manyata, amebainisha kuwa wananchi wanatakiwa kupata uelewa mpana na taarifa sahihi kwenye vyombo vya habari na kuchukua tahadhari ili kuepuka madhara ikiwemo kuugua kwa muda mrefu ama kifo kutokana na usugu wa vimelea vya magonjwa dhidi ya dawa (UVIDA).
Dkt. Manyata ameyasema hayo jana Desemba 30,2025, jijini Dar es salaam November 30, 2025, katika mafunzo maalum kwa Waandishi na Wahariri wa Vyombo mbalimbali vya Habari ikiwa ni sehemu ya mkakati na afua muhimu kulifanya kundi hilo ndani ya jamii kuwa mabalozi wa kukabiliana na madhara yatokanayo na UVIDA.
Ambapo amesema kuwa, Serikali kwa kushirikiana na wadau wamekuwa na mikakati mbalimbali kuweza kutoa elimu juu ya UVIDA ikiwamo kukutana na makundi yote katika Jamii nchini na wanahabari ni moja wapo.
Aidha, amebainisha kuwa, madhara ya UVIDA mtu anaweza kupata matibabu ya muda mrefu na yenye gharama, au pia hawezi kupona na hata uwezekano wa kusababisha kifo.
“Tunaweza kuepuka UVIDA kwa kuzingatia ushauri wa watalaam katika matumizi sahihi dawa. Pia kwa watu wa mifugo kupata taarifa sahihi na taratibu, usafi wa mazingira kuepuka magonjwa kama kuhara na kipindupindu,” amesema Dkt. Manyata.
Katika mafunzo, Dkt. Manyata ameweza kuelezea maeneo makubwa manne ikiwemo ufahamu dhidi ya UVIDA, na pia mikakati mbalimbali ya serikali ikiwamo kuwa na mpango maalum wa kampeni ya kila mwaka mwishoni mwa mwezi November (WAAW).

Katika mafunzo hayo ya UVIDA kwa waandishi wa habari na wahariri pia wadau wa mashirika mbalimbali yameweza kutoa elimu na namna wanavyoshirikiana na Serikali ndani na nje ya Afrika, mashirika hayo ni pamoja na Shirika la Afya Duniani (WHO) Kanda ya Afrika, Shirika la Afya la Wanyama Duniani (WOAH), Shirika la Mazingira (UNEP) Shirika la chakula (FAO) na Africa CDC.

