Bodi ya Michezo ya Kubahatisha yazindua kampeni kamata kamata mashine haramu za Dubwi

Na Mwandishi Wetu

BODI ya Michezo ya Kubahatisha Tanzania (GBT), kwa kushirikiana na Wenyeviti wa Serikali za Mitaa wa Mkoa wa Dar es Salaam, wamezindua kampeni maalum ya kutokomeza uchezaji wa mashine maarufu za dubwi  kinyume na utaratibu.

Kampeni hiyo iliyopewa jina la Fichua, Tukomeshe Mashine Haramu ilizunduliwa jijini jana ikienda sambamba na semina kwa washiriki ili kujua mashine ‘feki’ zinazotumika na kuipotezea taifa fedha.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Michezo ya Kubahatisha Tanzania (GBT), James Mbalwe, wamepokea malalamiko kutoka kwa wadau mbalimbali kuhusiana na kuenea kwa mshine za dubwi na kutumika kwa watoto chini ya miaka 18 ambapo ni kinyume na sheria.

Amesema mbali ya kutumika kwa watoto wadogo, pia mashine hizo zimewekwa kwenye nyumba za kuishi tofauti na baa au sehemu za burudani ambapo ni kinyume cha sheria.

“Pia wapo waliowahusisha watoto chini ya miaka 18 kucheza michezo ya kubahatisha, jambo ambalo ni kinyume cha kisheria ya nchi, ” amesema Mbalwe.

Amesema pamoja na kwamba mchezo wa dubwi upo kisheria, wapo wachezeshaji wanaouendesha kinyume cha sheria bila leseni na vile vile kutumia mashine zilizoingia nchini kwa njia ya ‘panya’. 

“Hawa ndiyo wanaosababisha sintofahamu hii huko mitaani, sasa kupitia kampeni hii, tutawasaka na kuwachukulia hatua za kisheria,” amesisitiza.

Kwa mujibu wa Mbalwe, michezo wa dubwi una maeneo yake maalumu ya kuwekwa mashine hizo ikiwamo kwenye baa na maeneo mengine ya starehe au burudani.

“Lakini kuna watu wanaziweka hadi majumbani mashine hizi za sloti (Dubwi) jambo ambalo si sawa kisheria na wanaofanya hivi ni wale wanaoendesha michezo hii kinyume cha taratibu bila kuwa na leseni za GBT.

Ili kutokomeza hili,  wamelazimika kushirikiana na wenyeviti wa Serikali za mitaa na pia kwa kushirikiana na wenzetu wa Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi).

“Hivyo, tumewapa wenyeviti wa Serikali za mitaa semina kuhusu uhalali wa mchezo huu, nani anastahili kucheza na eneo gani, hili tumelifanya kwa wenyeviti wa Serikali za mitaa wa Dar es Salaam ambako ndiyo kuna biashara kubwa ya michezo ya dubwi,  kisha tanakwenda mikoa mingine yote,” amesema.

Awali Mbalwe ametoa rai kwa wale wanaoshinda siku nzima wakicheza Dubwi bila kufanya kazi akisisitiza hiyo si afya kwa ustawi wa mchezaji.

“Tunafahamu mashine za sloti (dubwi) wanaochezesha kihalali ni wafanyabiashara kama wafanyabiashara wengine.

Washiriki mbalimbali, wakifuatilia semina iliyoandaliwa na Bodi ya Michezo ya Kubahatisha Tanzania (GBT) ambayo ilienda sambamba na uzinduzi wa kampeni hiyo.

“Wanafungua kama mtu anayefungua duka, lakini kwa wachezaji ni burudani hivyo wanatakiwa wacheze kwa kiasi, Bodi tunashauri wacheze kama burudani zingine, huwezi kufanya burudani kuanzia asubuhi hadi jioni, wacheze na wafanye kazi sio siku nzima wanashinda wakicheza dubwi,” amesema.

Kuhusu mchango wa michezo ya kubahatisha kwenye uchumi amesema inachangia uchumi wa nchi na maendeleo ya jamii.

“Inasaidia ajira na sekta ya michezo pia, timu zetu za taifa na ambazo si taifa zinanufaika kupitia michezo ya kubatisha kwani Serikali imetenga asilimia tano ya mapato ya michezo hii kusaidia moja kwa moja sekta ya michezo,” amesema.

Akielezea makusanyo ya kodi kwa mwaka uliopita, amesema iliyokusanywa kupitia michezo hiyo ni sh. bilioni 200.

“Mwaka huu tunatarajia zaidi ya sh. bilioni 250 hii ni kodi ya moja kwa moja, zipo kodi nyingine ikiwamo ile ya kuingiza mashine, ukiweka mapato na tozo na malipo mengine inaweza kufika zaidi ya sh. bilioni 250 bilioni hadi  sh. bilioni 300 bilioni,” amesema.

Akizungumzia kisheria, Meneja wa Leseni na Huduma za sheria wa GBT, Catherine Lamwai, amesema sheria inaipa bodi mamlaka ya kukamata na kuteketeza mashine ambazo hazipo kihalali.

Meneja wa Leseni na Huduma za sheria wa Bodi ya Michezo ya Kubahatisha Tanzania (GBT), Catherine Lamwai, akisalimia washiriki wakati wa semina na uzinduzi wa kampeni hiyo.

‘Mashine hizo ni zile ambazo muendeshaji hana leseni, mashine haina stika na imewekwa eneo ambalo sheria hailitambui ikiwamo ya makazi ya watu.

“Wanaochezesha dubwi kinyume cha sheria wakikamatwa tunawachukulia hatua ikiwamo kuteketeza mashine, hela zilizomo kutaifishwa na wao kufikishwa mahakamani kama waalifu wengine tukishirikiana na taasisi nyingine za serikali ikiwamo polisi, amesema Lamwai. 

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Wenyeviti wa Serikali za Mitaa Dar es Salaam, Juma Abbas, amesema wamepewa semina na GBT ambayo imewapa mwanga wa kutambua mashine za dubwi ambazo si sahihi.

“Mwanzo hatukuwa tukifahamu ipi ni sahihi na ipi si sahihi na mahala gani si sahihi michezo hii kufanyika, hatuwa tukijua tufanye nini kudhibiti hili japo malalamiko yalikuwa ni mengi huko mitaani.

“Sasa tuna ufahamu na jambo hili, tutalisimamia vizuri kuhakikisha mashine zilizopo zinaweka mahala sahihi na wachezaji wake ni wale tu wanaoruhusiwa kucheza kisheria, yule atakayekuwa na mashine hata kama yuko na leseni, akimchezesha mtoto hatutamfumbia macho,” amesema Abbas.

 hiyo.
Mmoja wa Wenyeviti wa Serikali ya Mitaa wa Mkoa wa Dar es Salaam, Saidi Kaunga, akionyesha kipaji chake cha kuimba akiwa na Bendi ya Mpoto wakati wa semina iliyoandaliwa na Bodi ya Michezo ya Kubahatisha Tanzania (GBT) ambayo ilienda sambamba na uzinduzi wa kampeni hiyo.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *