
Na Mwandishi Wetu, Tabora
MKURUGENZI wa Manispaa ya Tabora, Dkt. John Pima, amesema kuwa kiasi cha Sh. bilioni 19.9 zilizopelekwa mkoani humo kupitia mradi wa Uendelezaji Miundombinu ya Miji Tanzania (TACTIC) zimeleta mageuzi makubwa ya kiuchumi na kijamii kwa wananchi mkoani hapo.
Akielezea mafanikio hayo, Dkt. Pima amebainisha kuwa miundombinu inayotekelezwa chini ya mradi wa TACTIC ni pamoja na ujenzi wa Stendi, soko na ujenzi wa barabara zenye urefu wa kilomita 10.7 ambapo tayari ujenzi wa barabara umefikia asilimia 83.8. ya utekelezaji.
Amesema kuwa hapo awali miundombinu ya soko na stendi haikuwa rafiki kwa wafanyabiashara na wasafiri na kwamba kwasasa wanatengeneza mazingira mazuri kwao ili kuwavutia wawekezaji katika mkoa huo.
“Tabora inazidi kubadilika na kukamilika kwa miundombinu hii kutakuwa na manufaa mengi kwani licha ya kupendezesha na kukuza mji wetu, kutakuwa na mazingira mazuri kwa wafanyabiashara na nichukue fursa hii kuwakaribisha wadau mbalimbali kuja kuwekeza Tabora”, amesema.
Kwa upande wake, Meneja wa TARURA mkoa wa Tabora, Mhandisi Lusako Kilembe amesema kuwa Wakala huo umejipanga kufanya matengenezo ya barabara “maintanance” kwa wakati ili kuhakikisha zinadumu na kutoa huduma kwa wananchi.
” Tutatenga fedha katika bajeti zetu ili kuhakikisha matengenezo ya barabara yanafanyika kwa wakati kwani Serikali inatumia fedha nyingi kuzijenga”, amesema.
Baadhi ya wafanyabiashara katika Soko la Tabora wametoa maoni yao huku Bi. Mariam Aron akieleza kuwa matarajio yao nikuwa na mazingira mazuri ya kufanyia biashara pindi soko litakapokamilika.
“Matarajio yetu ni kuona miundombinu mipya ikiwemo vyoo vya kisasa ili tufanye biashara katika mazingira safi na salama hali itakayovutia wateja wengi na kukuza uchumi wetu”, amesema.
Bw. Maiko Kipeta ambaye ni mkazi wa Tabora na mfanyabiashara ameiomba Serikali kuhakikisha mradi wa soko unakamilika kwa wakati ili wafanyabiashara waanze kunufaika.
Mradi wa Uendelezaji Miundombinu ya Miji Tanzania (TACTIC) Manispaa ya Tabora unatekelezwa chini ya Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) pamoja Ofisi ya Mkurugenzi wa Manispaa ya Tabora ambapo kukamilika kwa mradi huo kutachochea maendeleo ya mkoa wa Tabora na kuwa kivutio kwa wawekezaji.

