TAMISEMI kutumia Bil. 66.57/- kujenga matundu ya vyoo 28,580 nchini

KATIKA mwaka 2025/26, Serikali imetenga Sh.Bilioni 66.57 kwa ajili ya kujenga matundu 28,580 ya vyoo katika shule za msingi na sekondari.

Akijibu hoja ya wabunge kuhusu serikali kufanya tathimini ya kubaini ubora na ukubwa wa tatizo la upungufu wa matundu ya vyoo katika shule zote za msingi na sekondari, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, Mohamed Mchengerwa amesema Serikali inatambua umuhimu wa kulinda afya za walimu na wanafunzi, hivyo itaendelea kukabiliana na changamoto hiyo kwa lengo la kulinda utu na afya za wanafunzi.

Amesema Sensa ya Elimumusingi ya mwaka 2024 inaonesha mahitaji ya matundu ya vyoo katika shule za msingi ni 429,599 wakati yaliyopo ni matundu 240,320, hivyo kuwa na upungufu kuwa ni matundu 189,279, hivyo kufanya wastani wa uwiano kwa wavulana ni 1:47 badala ya 1:25 unaohitajika na kwa wasichana kuwa ni 1:43 badala ya 1:20.

Kwa upande wa sekondari, mahitaji ni matundu 135,870 wakati yaliyopo ni matundu 84,608 na upungufu ni matundu 51,262, hivyo kufanya wastani wa uwiano uliopo kwa wavulana ni 1:36 badala ya 1:25 na wasichana ni 1:35 badala ya 1:20.

Aidha, Mchengerwa amesema mkakati wa Serikali ni kufanya tathmini ya ubora wa ujenzi wa matundu ya vyoo na kuendelea kutenga fedha kila mwaka kwa ajili ya ujenzi wa matundu ya vyoo kwa shule za msingi na sekondari na kuhakikisha kuwa kwa sasa kila darasa linalojengwa kunakuwa na ujenzi wa angalau matundu mawili ya vyoo.

“Katika mwaka 2025/26, Serikali imepanga kujenga matundu 28,580 ya vyoo yatakayogharimu shilingi bilioni 66.57 katika shule za msingi na sekondari.”
Mchengerwa ameongeza kuwa: choo cha staha ni haki ya mwanafunzi; ni chozi lisiloonekana, lakini lenye kuumiza.”

“Tuwashe mwenge wa heshima shuleni-tuzime giza la aibu ya vyoo visivyofaa…Serikali haijalala katika hili, lengo ni kuhakikisha shule zetu zinakuwa mahali salama pa fundishia na kujifunzia,” amesema.


Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *