
Na Mwandishi Wetu
Wakala wa Nishati Vijijini (REA) umeitambulisha Kampuni ya Manjis Gas ambayo imepewa jukumu la kusambaza mitungi ya gesi 22,785 itakayouzwa kwa bei ya ruzuku ya asilimia 50 katika Mkoa wa Pwani.
Hayo yamebainishwa jana Aprili 16, 2025 katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoani Pwani na Ofisa Maendeleo Mwandamizi kutoka REA, Jaina Msuya, wakati wa uwasilishwaji wa taarifa ya utekelezaji wa mradi wa usambazaji mitungi ya gesi yenye ujazo wa kilo sita mkoani humo.
Msuya amesema kuwa mitungi ya gesi 22,785 itakayosambazwa mkoani Pwani ni utekelezaji wa Mkakati wa Kitaifa wa Nishati Safi ya Kupikia ambao una lengo la kuongeza matumizi ya nishati safi kufikia asilimia 80 ifikapo 2034.
“Lengo la mradi ni kuongeza upatikanaji wa huduma za nishati safi ya kupikia kwa kuwawezesha wananchi wengi kumudu gharama za bidhaa za nishati safi ili kutunza mazingira, kuokoa muda ili wananchi na jamii kwa ujumla kushiriki katika shughuli mbalimbali za kuiuchumi, kijamii ikiwamo siasa nakupunguza maradhi ya upumuaji na macho,” Amesema Msuya.
Ameongeza kuwa gharama ya Mradi huo ni Sh. 398,737,500.
Amezitaja wilaya zitakazonufaika kuwa ni pamoja na Wilaya ya Bagamoyo, Kibaha, Rufiji, Kibiti, Mkuranga, Kisarawe na Mafia. Kila wilaya itapata mitungi 3,255.
Kwa upande wake, Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Songwe, Shangwe Twamala ameipongeza REA kwa kuja na mradi huo na kuiomba iwe endelevu ili iweze kuwasambazia wananchi wengi nishati hiyo muhimu.
Naye Mwakilishi kutoka kampuni ya Manjis gas, Gracious Maimu amesema watatekeleza mradi huo kwa kuzingatia makubaliano ya Mkataba wa kusambaza mitungi ya gesi ya kupikia pamoja na kutoa elimu na kuhamasisha wananchi ili wingi ili kuchochea matumizi ya nishati hiyo.