Serikali kuzindua Sera Mpya ya Biashara

SERIKALI inatarajia kuzindua Sera mpya ya Taifa ya Biashara ya 2003 Toleo la 2023 yenye dhamira ya kuweka mfumo na mkakati madhubuti unaolenga kuboresha mazingira ya biashara, kuongeza ajira, Pato la Taifa, ukuaji wa kiuchumi na kuboresha ustawi wa wananchi.

Sera hiyo mpya imeoanisha sera na kanuni za biashara na sera zinazohusiana na masuala ya kibiashara, kuondoka mgongano wa kisheria, mgawanyo wa majukunu ya kitaasisi, kuimarisha miundombinu ya masoko na biashara, kupunguzwa muda na gharama za ufanyaji biashara, kuwezesha biashara mtandao, biashara ya huduma, usimamizi wa ushindani halali wa kibiashara na kumlinda mlaji.

Waziri wa Viwanda na Biashara Dkt. Selemani Jafo, ameyasema hayo Julai 28, 2024 Dar es Salaam alipokuwa akiongea na Waandishi wa Habari kuhusu uzinduzi wa Sera hiyo utakaofanyika Julai 30, 2024 jijini Dar es Salaam.

Aidha, amebainisha kuwa Mgeni Rasmi katika uzinduzi wa sera hiyo inayoongozwa na kauli mbiu isemayo “ushindani wa biashara katika kuchochea kasi ya mabadiliko ya kijamii na kiuchumi yanayoongozwa na viwanda” anatarajiwa kuwa Naibu Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Waziri wa Nishati Dkt. Dotto Biteko

Vilevile amebainisha kuwa hafla hiyo ya uzinduzi inajumuisha wadau mbalimbali wapatao 300 kutoka Taasisi za umma, Taasisi Binafsi, Mashirika ya Dini, Wabia wa Maendeleo, Mabalozi, Vyama vya Wafanyabiashara na wenye Viwanda na Wafanyabiashara.

Naye Mkurugenzi mkazi wa kampuni ya Trade Mark Afrika Elibariki Shammy aliipongeza Tanzania kwa kufanya maboresho hayo na kusisitiza kuwa ni vema kila Nchi ya Afrika liige hatua hiyo ili biashara ziweze kufanyika kwa urahisi kwa kuwa bado Sera nyingi zinakinzana

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *