PROF. MKUMBO: TAFITI ZIHUSISHE SEKTA BINAFSI KUCHOCHEA UBUNIFU

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
WAZIRI wa Mipango na Uwekezaji, Prof. Kitila Mkumbo, amekitaka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) kuendelea kushirikiana na sekta binafsi ili kuimarisha tafiti na kuchochea ugunduzi wa kiteknolojia nchini.

Waziri Mkumbo ametoa wito huo jana Juni 9, 2025 jijini Dar es Salaam wakati akizindua Maonesho ya 10 ya Utafiti na Ubunifu yanayolenga kuhamasisha matumizi ya teknolojia katika kuharakisha ubunifu wa kitaifa.

Akizungumza katika uzinduzi huo, Prof. Mkumbo, amesema kuwa tafiti zinazofanywa na vyuo vikuu zinapaswa kuangalia namna ya kuchangia maendeleo ya kiuchumi katika sekta mbalimbali ikiwamo viwanda, biashara, usafiri na taasisi za kifedha.

Ameeleza kuwa kutokana na mabadiliko ya kisera katika baadhi ya nchi wahisani, ambapo kumekuwa na kupungua kwa ufadhili wa tafiti, chuo hicho kinapaswa kujikita zaidi kwa wadau wa ndani.

Hata hivyo, amesema serikali itaongeza nguvu katika kusaidia tafiti na ipo kwenye mpango wa kutenga asilimia moja ya pato la Taifa kwaajili ya kuendeleza tafiti nchini.

Kwa upande wake, Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam – Utafiti, Prof. Nelson Boniface, amesema chuo kimefanikiwa kushirikiana na wadau tisa kutoka sekta ya teknolojia, benki na kampuni za simu ambao wamewezesha upatikanaji wa fedha kwaajili ya kusaidia tafiti mbalimbali kwa kipindi cha miaka 10 iliyopita.

Prof. Boniface amewataka wananchi kujitokeza kwa wingi katika maonesho hayo ili kujionea kwa vitendo namna teknolojia za kidijitali zinavyoweza kutumika katika biashara, elimu, na kutatua changamoto mbalimbali za kijamii.

Maonesho hayo yameanza jana Juni 9 na yanatarajiwa kufungwa kesho Juni 11, 2025, yakiwa yamebeba kaulimbiu isemayo: “Kutumia Teknolojia za Kidijitali: Katika Kuharakisha Ubunifu na Tafiti.”

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *